08/04/2022
MY STORY; MKE WANGU SITAKI UPUMZIKE KWA AMANI!
Ni miezi miwili tangu nimzike mke wangu, nyumba imekua kimya sana, pamoja na kukaa naye kwenye ndoa kwa miaka 7 leo ndiyo k**a nimegundua kuwa nilikua na mke.
Wakati wote wa ndoa nilikua namuona k**a lidubwasha flani tu lipo kunijazia choo. Nilishamfukuza mara nyingi, nilishampiga mara nyingi nikimuambia kuwa hana akili, mjinga kaja kunijazia choo tu hana faida.
Kusema kweli sikuwahi kuwaza k**a itakuja kutokea siku k**a hii ya leo nikatamani kuwa na mke wangu. Ndugu zangu walikua ndiyo kila kitu kwangu, hasa dada yangu mkubwa, kaolewa lakini kila siku alikua anakuja kwangu.
Anakagua nyumba na kuniambia ni chafu, naishia kumpiga mke wangu kumuambia kazi yake ni kula na kunya tu hata kufanya usafi hawezi.
Niulishamnyang’anya watoto na kuwapeleka kwa dada yangu, wanakaa muda nawarudisha, nilishamlaza nnje mara nyingi, nikampiga mbele ya watoto.
Niliwakataza mpaka wanangu kumuita Mama, ni kawaambia mtu mwenye hadhi ya kuitwa Mama ni mama yangu tu yeye ni mjinga hapaswi kuitwa Mama. Nikataka wamuite kwa jina lake. Lakini miezi miwili iliyopita kila kitu kilibadilika, niliamka asubuhi k**a kawaida yangu nikiwaza kwenda kazini.
Mke wangu hakua kitandani, sikushangaa yeye kutokua kitandani ila nilishangaa kwanini hajaniamsha wakati jua lilishaanza kuwaka.
Nilintanyuka huku nikitukana, nikaenda sebuleni nakuta watoto bado hawajaandaliwa, jikoni simuoni, nikarudi chumbani huku nikitukana.
Naingia bafuni namkuta kalala, nahisi labda kachoka kajilaza, naanza kumpiga huku nikimtukana ili anyanyuke ila hakunyanyuka.
Alikua ameshakauka muda mrefu, hata hakuonekana kudondoka bali kukaa. Naita watu, mwili unachukuliwa, Baada ya vipimo kumbe presha ilipanda, mishipa ya kichwa ikapasuka.
Naumia zaidi kwakua usiku wake nilikua namtishia aondoke kwani aliedna hospitalini kupima ana ujauzito ambao ingawa nilijua kuwa ni wangu ila nilimuambia si wangu atafute mwanaume wakumpa. Sikumgusa usiku huo, si kwakua sikutaka ila nilikua niemchoka sana, kumtukana tu nilimtukana.
Mke alizikwa, nilijikaza silii, nilikua sioni umuhimu wake. Lakini miezi miwili tu, mke wangu kafariki, kila siku nilikua namuambia aondoke anichie watoto leo kaondoka, kaniachia, baada ya mazishi niliwapaleka kwa Dada ila leo kawarudisha anasema kazi zimemzidia nitafute mfanyakazi.
Dada yuleyule aliyekua akiniambia “Aondoke kwani alikuja na na watoto, wanao ni damu yetu tutalkea!” Leo miezi miwili tu mke wangu kaondoka hakuna hata ndugu anayekuja kunisalimia.
Nimekaa mwenyewe na wanangu, kila dakika wanamuulizia Mama yao na sijui cha kuwajibu. Mke wangu nionyeshe ishara nifanye nini na hawa watoto, Mama kaniambia niwapeleke Kijijini lakini naona ugumu kwani umri wake mkubwa na kule maisha ni magumu.
Nataka kumleta kwangu akae na wajukuu zake lakini hataki kuondoka kijijini. Mke wangu ni k**a umeondoka na kila kitu, umeondoka na furaha yangu, kila mtu kanigeuka mke wangu. Natamani hata ningekuonyesha upendo.
Vile vitu vyote nilivyokua nakunyanyasia mke wangu, nyumba, gari ambayo hukuwahi kuipanda, miaka minne mimi mume wako nilikua na gari lakini ulipanda Bajaji, hukuwahi kuipanda hata siku moja ila ndugu na marafiki nilikua nawaazima waitumie.
Mke wangu leo ndiyo nimejua nakupenda, sioni hata sababu ya kuamka tena. Natamani sana hata ungejua nijinsi gani nilikua nakupenda, nilishindwa kukuonyesha upendo, najua unaweza usiamini ila naumia na sijui maisha yangu bila wewe yatakuaje.
Ningesema upumzike kwa amani ila sitaki upumzike mke wangu. Naomba hata unisaidie kuela hawa watoto, waambie kitu wanyamaze. Nilijitahidi Sana wakuchukie kila dakika wanakuita wewe, nisaidie mke wangu usipumzike kwanza.
MWISHO