14/11/2025
TAMBUA MAHITAJI MUHIMU YA KUZINGATIA UNAPOANZA KUSTAAFU KUWA MTUMISHI WA UMMA AU SEKTA BINAFSI:
Kujiandaa kustaafu ni hatua inayojumuisha kujiandaa katika masuala ya uwekaji akiba, uwekezaji na kisaikolojia na masuala ya kijamii kwa lengo la kuwa na kipato cha kutosheleza mahitaji katika kipindi mtumishi anapostaafu ili kuishi maisha ya staha ukiwa nje ya utumishi au ajira. Uzoefu unaonesha kwamba watumishi au wafanyakazi wengi huanza maandalizi ya kustaafu miaka michache kabla ya kustaafu na wengine hata husubiri hadi siku ya kustaafu lakini inashauriwa mtumishi kuanza maandalizi angalau miaka 15 kabla ya kufikia kipindi cha kustaafu au mara baada ya kuajiriwa.
Leo, tunaangazia mahitaji muhimu kwa mtumishi kuyazingatia wakati akijiandaa kustaafu. Mtumishi anapojiandaa kustaafu anapaswa kupitia gharama za maisha kabla ya kustaafu na gharama za maisha zitakavyokuwa baada ya kustaafu. Mapitio ya gharama za maisha zitawezesha mtumishi kuweza kuwa na makisio ya kipato kinachohitajika kugharamia maisha baada ya kustaafu. Kwa mfano wataalam wa fedha wengi wanakadiria kwamba mtumishi atahitaji asilimia 70 hadi 90 ya kipato chake kabla ya kustaafu ili aweze kugharamia maisha yake baada ya kustaafu. Suala hili ni muhimu kwa sababu ukweli ni kwamba mtumishi anapostaafu kipato chake hupungua na kipato kutoka Mifuko ya hifadhi ya jamii hakitoshelezi kugharamia matumizi kwa watumishi walio wengi kulingana na mtindo wao wa maisha (matumizi makubwa kuliko kipato).
Nikukumbushe kwamba gharama za maisha baada ya kustaafu, zinategemea na mtindo wa maisha yako utakavyokuwa, kwa hiyo unapoanza kujiandaa kustaafu ni muhimju kuanza pia kufanya maboresho ya mtindo wa maisha ili kuepuka kuwa gharama kubwa ya maisha baada ya kustaafu. Aidha, unapoanza kujiandaa kustaafu fanya tathmini ya hali yako ya madeni ili uweze kustaafu ukiwa na madeni machache au kutokuwa na madeni kabisa ili kuepuka kuathiri uwezo wa kugharamia familia.
Fanya thathmini ya mahitaji ya kiafya baada ya kustaafu kwa sababu maisha ya uzeeni au baada ya kustaafu yanahusisha matatizo ya kiafya mengi k**a vile Shinikizo la Damu, Kisukari, Matatizo ya Miguu n.k, hivyo usipoweka mpango thabiti wa maisha yako baada ya kustaafu utapata changamoto sana kugharamia matibabu n.k. Pia, kuna eneo muhimu la kujiandaa kisaikolojia, kwa sababu mambo mengi hubadilika baada ya kustaafu mfano, kipato kitapungua, hutakutana mara kwa mara na watumishi wenzako n.k kwa hiyo ni lazima kuanza kujiandaa kisaikolojia kwa kutafuta washauri wa kisaikolojia mapema.
Fanya tathmini ya wingi wa wategemezi au jinsi unavyotegemewa kiuchumi na ndugu, jamaa na marafiki ili kujua unahitaji kiwango gani cha kipato ili kuweza kugharamia mahitaji hayo kutoka kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki. Suala hili ni muhimu kuzingatia kwa sababu, watumishi waliowengi husaidia ndugu katika kulipa ada na mahitaji mengine ya kijamii, k**a utaendelea na utaratibu huo utahitaji kuwa na uwezo wa kufanikisha hilo.
Unapoaza kujiandaa kustaafu unapaswa pia kufikiria kuhusu uwekezaji katika shughuli mbalimbal ambazo utazifanya ukiwa umestaafu. Katika kutekeleza hili, kamwe usisubiri kuwekeza ukiwa umestaafu tayari, uwezekano wa kupoteza utakuwa mkubwa sana kwa sababu utakuwa hauna uzoefu na taarifa muhimu za hiyo shughuli au biashara unayotaka kuwekeza. Aidha, unapofikiria kuwekeza weka kipaumbele kwa uwekezaji utakaokupa kipato tulivu (passive income) kwa kuwekeza katika maeneo ambayo hayakuhitaji uwepo ili kuingiza kipato.
Fanya uamuzi makazi yako yatakuwa wapi baada ya kustaafu nikimaanisha utaishi mjini au utaishi kijijini au nje ya mji? Eneo utakaloishi lina athari katika gharama ya maisha baada ya kustaafu na aina ya shughuli utakayofanya baada ya kustaafu. Mfano ukiishi mjini, gharama za usafiri, chakula ni kubwa ukilinganisha na ukiishi kijijini, pia shughuli k**a za kilimo na ufugaji utazifanya vizuri ukiwa kijijini. Kwa hiyo, maamuzi ya utaishi wapi baada ya kustaafu yanaweza kuwa na faida au hasara kwako.
Mwisho kabisa , mtumishi unapaswa kufikiria kuhusu maisha ya kijamii katika maeneo yetu tunayoishi kwa sababu ukweli ni kwamba watumishi tunatumia muda mrefu tukiwa kazini kwa lugha rahisi nikwamba tunaishi kazini na kulala nyumbani. Hali hiyo, inasababisha kutokuwa na mahusiano na wanajamii wanaotuzunguka, kutoshiriki katika matukio mengi ya kijamii na kuonekana k**a tunaishi maisha ya kujitenga, kujisikia n,k. Kwa hiyo, unapoanza kujiandaa kustaafu anza kuimarisha mahusiano na jamii yako kwa kushiriki katika matukio muhimu ili unapostaafu uweze kuishi vizuri na jamii yako, kwa sababu ukistaafu maisha yako yatakuwa katika mazingira yako ya nyumbani.
Kwa mialiko ya kibiashara (Mafunzo/Semina/Kongamano n.k) tafadhali usisite kutupigia simu 0672619660, tutakufikia Mkoa/Wilaya/Mji wowote hapa Tanzania kwa gharama utakazomudu.