13/04/2026
BARAZA LA WAFANYAKAZI ASA LAPITISHA BAJETI YA WAKALA KWA MWAKA WA FEDHA 2026/2027.
Baraza la Wafanyakazi la Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) limepitisha mapendekezo ya Mpango na bajeti kwa mwaka wa fedha 2026/2027, ikiwa ni hatua muhimu katika kuimarisha uzalishaji na upatikanaji wa mbegu bora nchini.
Akiwasilisha mapendekezo hayo Leo tarehe 13 April 2026 jijini Morogoro, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi, Bi. Mary Machaku, amesema kuwa bajeti hiyo inalenga kugharamia shughuli za Uendeshaji wa Taasisi, Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo pamoja na kuongeza ufanisi wa mapato ya ndani ya Wakala.
โASA imepanga kutekeleza vipaumbele mbalimbali vyenye lengo la kuongeza uzalishaji wa mbegu bora za kilimo kufikia Tani 27,200, kuimarisha usambazaji ili kuwafikia wakulima kwa wakati na ujenzi wa uzio wa kilomita 158.5 katika mashamba mbalimbali ya ASAโ amesema Bi. Machaku
Aidha, Akiahirisha kikao hicho kwa niaba ya Mtendaji Mkuu, Bw. Leo Mavika, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara, Dkt. Basili Msuha, amesema ASA itaendelea kushirikiana na wakulima wa mkataba ili kuhakikisha uzalishaji wa mbegu bora unaongezeka kwa kuzingatia viwango vya ubora.
โKupitia bajeti hii, ASA imejipanga kuhakikisha mbegu zinapatikana kwa wakati kwa wakulima ili kuongeza tija katika Sekta ya kilimo na nahimiza watumishi wote kufanya kazi kwa bidii na kujituma ili kufanikisha malengo yaliyowekwa,โ amesema Dkt. Msuha.
Baadhi ya wajumbe wa Baraza hilo walichangia na kutoa maoni kupitia bajeti hiyo kwa kueleza kuwa inaonesha mwelekeo chanya katika kukuza uzalishaji wa mbegu bora na kuchangia maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.
Katika hatua nyingine, Baraza lilifanya uchaguzi mdogo wa Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi na kumchagua ndugu Erick Iramba kuwa Katibu Msaidizi wa Baraza la wafanyakazi la ASA, kufuatia kifo cha aliyekuwa Katibu Msaidizi wa Baraza hilo, ndugu Constantine Nzila, kilichotokea mwaka 2025.